Bidhaa za China zinavyotamba kwenye soko la Tanzania
Wiki mbili zilizopita katika sehemu ya kwanza ya makala haya ya ‘Dar hadi China’ tuliona jinsi wakuu wa mataifa haya mahili wanavyoimarisha uhusiano na kuwakutanisha pamoja wafanyabiashara wa mataifa haya mawili. Tukaona pia umuhimu wa wafanyabiashara pande zote kuwa huru katika kuimarisha ushirikiano wa kibiashara.
Leo tunakutana na wafanyabiashara wa Tanzania
wanaelezea juu ya kile ambacho kinawavutia katika kununua na kuuza
bidhaa za China. Yamekuwapo maneno mengi kuhusu bidhaa za China.
Wafanyabiashara na wanunuzi wa Tanzania wana nini cha kusema?
Ushindani wa bidhaa mbalimbali za biashara, zikiwapo zinazotoka nje ya nchi, unazidi kukua siku hadi siku nchini.
Kila kukicha wafanyabiashara wanaumiza vichwa jinsi ya kumudu ushindani huo kwa kubuni mbinu mbalimbali za kuwavutia wateja wao.
Kutokana na ushindani huo, wafanyabiashara
hutafuta bidhaa zinazopendwa na wateja wengi. bidhaa hizo, huzinunua
kutoka kwa wazalishaji wa ndani na nje.
Miongoni mwa mataifa ya nje ambayo bidhaa zake huingizwa na kuuzwa kwa wingi nchini ni China.
Kariakoo ni eneo kuu la biashara nchini ambalo
linategemewa na mikoa yote nchini kupata bidhaa mbalimbali. Ni eneo
ambalo twaweza kusema ni lango la kuingiza bidhaa za aina mbalimbali
nchini kwa kuwa wafanyabiashara wa mikoani hununua vitu na kwenda
kuviuza wanakotoka.
Eneo la Kariakoo lililopo Jijini Dar es Salaam,
linaelezwa kuwa na asilimia kubwa ya bidhaa zinatoka China. Hizi ni kama
vile nguo, viatu, mapambo, vifaa vya umeme, ujenzi, michezo, pikipiki,
bajaji na samani. Bidhaa hizi zinatumiwa na Watanzania wengi.
Bob Lema ni mfanyabiashara katika soko hilo.
Amekuwa akifanya biashara ya kuuza vifaa vya umeme kwa kipindi cha miaka
10 sasa. Anasema uzoefu wake katika biashara hiyo unaonyesha kuwa
bidhaa nyingi zinazoingizwa kutoka nje ni zile za China.
“Tunanunua bidhaa kutoka nchi mbalimbali, lakini
China inaongoza. Huo ni mtazamo wangu na jinsi ninavyofahamu soko la
biashara lilivyo hasa hapa Kariakoo,” anasema Lema huku alionyesha
baadhi ya vifaa vya umeme alivyonunua kutoka China.
“Unaona kama hizi spika, zinaitwa ‘skeleton
speakers’ zipo za Marekani na China. Lakini palee (anaonyoshea nyingine)
zile ni za China. Halafu kuna televisheni zote hizo zinatoka China.”
Anasema, nchi hiyo inajitahidi kuzalisha bidhaa nzuri na zenye gharama nafuu ambazo watu wengi wanazimudu.
“Unaona kama hizo spika nimekuonyesha ubora wake
ni sawa lakini tunazonunua kutoka Marekani ni ghali zaidi. Kuna tofauti
kidogo ya bei,” anasema.
Lema anaainisha kuwa kwa upande wa ubora huwa kuna wakati mwingine wazalishaji wanakuwa na bidhaa zenye upungufu.
“Kama ilivyo kwa bidhaa au huduma nyingine. Kuna wakati unaweza kuteleza ukaboronga basi na kwao ndiyo inakuwa hivyo.”
Anabainisha kuwa ndiyo maana mteja anapewa muda kile kitu alichonunua kikiwa na kasoro anarudisha na kupewa kingine.
Kwa sababu hiyo, anasema wateja wanapenda bidhaa
za China kwakuwa ni za bei nafuu na hazina tofauti kubwa na bidhaa za
mataifa mengine ambazo zinauzwa kwa bei kubwa.
Wakati anatoa maelezo hayo, aliingia mteja
aliyekuwa anahitaji jenereta. Katika maongezi nilitaka kumdadisi ili
kufahamu kama aliwahi kununua bidhaa ya China na anazizungumziaje.
Mteja huyo aliyejitambulisha, Aron Daniel anasema
kuwa, aliwahi kununua televisheni aina ya Sony miaka mitatu iliyopita na
haijawahi kupata matatizo ya kiufundi.
“Hiyo TV naitumia hadi leo na imetengenezwa kutoka
China. Wala siyo hiyo tu zipo bidhaa nyingi za China natumia nyumbani
na hazijawahi kuwa na matatizo ya kiufundi.
“Hata yakitokea ni ya kawaida kama ilivyo kwa
bidhaa zinazozalishwa kutoka nchini nyingine. Kama zingekuwa na
matatizo, ningekuwa narudi hapa kila siku kwa sababu hapa ndipo
ninaponunulia vifaa vyangu vya umeme,” anabainisha Daniel.
Ofisa Masoko wa duka la simu za Nokia, John
Stewart anasema: “Unajua sasa hivi watu wameelimika. Walikuwa wanasikia
bidhaa za China ni feki lakini mtu anapokuja kununua kitu kama simu
dukani, ukampa waranti ya mwaka au miezi sita akaenda kutumia kwa muda
mrefu bila kumsumbua, lazima ataamini bidhaa yako.”
“Nakupa mfano wa Nokia Lumia. Hizo simu
zinazalishwa China lakini ndiyo simu zinazonunuliwa kwa wingi sasa hivi
kwa sababu ya ubora wake.” Anaongeza: “Asilimia 80 ya bidhaa zinazouzwa
sokoni hapa ni zile zinazozalishwa China. Watu wengi sana wananunua
bidhaa za China. Ni nafuu na ni bora.”
Lakini, ofisa huyo anatoa angalizo kuwa wapo baadhi ya
wafanyabiashara wakubwa ambao huenda China na kuomba watengenezewe
bidhaa ambazo hazina ubora kwa gharama ndogo.
“Hao ndiyo wanaoharibu kwa sababu zile bidhaa
zikiingizwa nchini zinaonekana hazina viwango. Lakini bila hivyo bidhaa
zao ni nzuri tu ndiyo maana zinatumika na mataifa mengine pia,”
anabainisha Stewart.
Mmiliki wa duka la Lelah Clothing, Leila Ally anazungumzia upande wa mavazi yanayozalishwa China na kuuzwa nchini.
“Ubora wa bidhaa unatokana na mnunuaji anataka
nini. Mimi siwezi kuagiza bidhaa mbaya wakati nafahamu fika walaji wangu
wanahitaji kitu cha namna gani,” alisema.
“Kama mfanyabiashara hadi nachukua uamuzi wa
kununua bidhaa zao na kuleta huku ni dhahiri kuwa hizo bidhaa ni nzuri
na zinafaa wateja wangu na wakinunua watakuja tena na tena kununua.
Tunapozungumzia bidhaa za China tunazinunua sana na walaji pia wapo
wengi. Hizo nyingine feki ni changamoto za kawaida tu katika biashara.”
Kauli hiyo inaungwa mkono na Victoria Ruga, ambaye
alikuwa dukani hapo ananunua nguo. “Wakati mwingine watu wanaongea kwa
sababu ya ushabiki lakini mimi sidhani kama yote ni ya kweli. Nguo zao
ni nzuri na kuna wakati mapungufu (upungufu) hayaepukiki na yanaweza
kurekebishika.”
Ally Ramadhani, muuzaji wa pikipiki anabainisha
kuwa aina za bajaji ambazo hutoka China zimekuwa zikinunuliwa kwa wingi
ukilinganisha na zile zinazotoka nchini nyingine. Anasema kuwa hata
vipuri vyake kwa sasa vinapatikana kwa wingi.
Ni kutokana na sifa hizo bidhaa za China zinazidi
kujijengea umaarufu nchini huku mamlaka za kudhibiti ubora kama vile
Shirika la Viwango Tanzania (TBS) likikabiliana na wale wanaoingiza
zisizo na viwango.
0 comments:
Post a Comment